Monday, March 3, 2014

Mapya Yaibuka Bunge la Katiba, TEC Yawaonya Wabunge..!

 
Mwenyekiti wa Muda Bunge Maalumu la Katiba, Pandu Kificho.
Mwenyekiti wa Muda Bunge Maalumu la Katiba, Pandu Kificho.

TUME ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), imetoa tamko ikitaka Bunge Maalumu la Katiba kuepuka kukashifu mapendekezo ya muundo wa Serikali tatu. TEC imesema muundo wa Serikali mbili haukutatua matatizo ya msingi na badala yake ulilimbikiza kero zilizosababisha Zanzibar kujiundia Katiba yake mwaka 2010 bila kushauriana na Tanzania Bara.
Tamko hilo limesainiwa na Mwenyekiti wa tume hiyo, Askofu Mkuu, Paulo Ruzoka. Tume hiyo imesema pendekezo la Serikali tatu litawarudisha Watanzania hali ya kuwa na umoja.
“Pendekezo la Serikali tatu lililowekewa mazingira tekelezi yakitoa mwanya wa kuboresha muundo huo kwa njia ya uwazi, shirikishi na za kidemokrasia lina tija kubwa ya kuturudishia umoja,” limesema.
Tamko hilo la kurasa 15 limetolewa baada ya mkutano wa kitaifa wa wajumbe wa Kamati za Majimbo za Haki na Amani za kanisa hilo na Chama cha Wanataaluma Wakatoliki Tanzania (CPT), uliofanyika Februari 5 na 6 mwaka huu jijini Dar es Salaam.
CPT ambayo imekuwa ikitumika kutoa matamko ya Kanisa Katoliki nchini na kuibua mijadala mizito, imesambaza tamko hilo kwa wajumbe wa Bunge la Katiba ambao ni marafiki wa chombo hicho, ikiwaomba walitumie tamko hilo kutafakari wakati wakijiandaa na mijadala katika Bunge hilo.
Tume hiyo ya TEC imesema baada ya kuchambua Rasimu ya Pili ya Katiba, wajumbe wa mkutano huo waliridhia kuwa Katiba inayoandaliwa si ya wanasiasa, vyama vya siasa wala asasi za kidini.
“Katiba yetu isiruhusu wachache wenye nguvu ya kisiasa, kiuchumi na kiutawala kutumia vibaya uwezo wao na kusababisha utengano kitabaka,” limesisitiza tamko hilo.
Tamko hilo limesema pendekezo la muundo wa Muungano wa Serikali tatu si jambo kuu kuliko mengine yote katika rasimu hiyo na kusisitiza kuwa Bunge lisikashifu mapendekezo hayo.
“Rasimu ya pili ni hatua njema katika tukio muhimu na la kihistoria nchini Tanzania. Tunatarajia Bunge Maalumu lisimkane Mungu na lisikashifu mapendekezo ya Serikali tatu,” limesema.
Kanisa hilo limesema duniani hakuna Katiba yoyote kamilifu na kwamba Watanzania waanze na rasimu iliyopendekezwa na Katiba hiyo iendelee kuboreshwa pale itakapobidi.
“Tunawaalika wananchi wote wa Tanzania kwa dhamira moja, kuliombea na kulisaidia Bunge Maalumu la Katiba liweze kufanya kazi yake kwa ustadi na kujali masilahi ya taifa,” limesema tamko hilo.
Tamko hilo limekuja wakati Bunge la Katiba likiwa njia panda kutokana na wajumbe wake kuyumbishwa na misimamo ya vyama.
Wajumbe hao wameshindwa kuafikiana kuhusu namna ya kupiga kura wakati wa kupitisha vifungu vya Katiba, huku CCM ikishikilia msimamo wa kutaka kura ya wazi na makundi mengine kura ya siri.
Kabla ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2010, taasisi hiyo ya kidini ilitoa matamko mawili, moja juu ya sifa za viongozi wanaostahili kuchaguliwa na jingine la ilani ya uchaguzi ya kanisa hilo, mambo ambayo yaliibua mijadala mizito.

No comments:

Post a Comment