Monday, November 4, 2013

MAKALA:TANZANIA TUNAONEWA AMA HATUJAPELEKA WAIMBAJI WENYE VIPAJI TUSKER PROJECT FAME?



Imeandikwa na Bongo5.com
Kwanza kabisa, naomba nijilaumu kwa kuwa na matarajio mengi kwa wawakilishi wa Tanzania kwenye msimu huu wa shindano la Tusker Project Fame. Ndio maana waliosema ‘Less expectation, Less hurt, don’t expect too much’ ama ‘too much expectation leads to disappointment’ hawakuwa wajinga.


Niliandika tweet hiyo kwa kujiamini mno kwakuwa naufahamu uwezo wa Tanah na Angel hata kabla ya hapo.

Nani asiyeijua sauti tamu ya Angel kwenye wimbo wa Ommy Dimpoz, Baadaye? Utamu wa sauti yake, ndio uliichanganya hadi academy ya Kili Music Awards imtaje mwaka huu kuwania kipengele cha Msanii Bora Anayechipukia, pamoja na kwamba hajawahi kutoa wimbo wake mwenyewe.

Kama umewahi kusikiliza nyimbo za kundi la Tanchy linaoundwa na Tanah na Chibwa, bila shaka utakuwa na picha kidogo ya uwezo wa Tanah.

Nitaanza kumzungumzia kwanza Tanah aliyeanza kutolewa kwenye shindano hilo wiki ya kwanza tu. Nilisema wazi, kutolewa kwa Tanah kulikuwa kwa uonevu zaidi kuliko kwa washiriki wengine hasa kwakuwa siku hiyo aliimba vizuri kuwazidi washiriki wengi tu waliobakia kwenye academy.

Nilikuwa na uhakika na bado ntaendelea kuwa na msimamo huo kuwa, Tanah alionewa. Ama tuseme alichukuliwa poa, na masikio ya majaji yalilazimisha kumsikia tofauti? Ama pengine chaguo la wimbo wa Alicia Keys, ‘No One’ aliouimba siku hiyo lilishindwa kumpa wigo mpana wa kukinadi kipaji chake? Lakini nahisi, wakati mwingine, majaji na walimu wanapaswa kutoa hukumu kwa kuangalia mengi zaidi ya uchaguzi mbaya wa wimbo. Ni rahisi kukitambua kipaji cha mtu, hata kama wimbo aliouchagua utamnyima fursa ya kutoa kile anachoweza kukifanya.

Nakubali kuwa, ni rahisi mimi kusema hivyo kwakuwa naujua uwezo wake tofauti na ule aliouonesha kwenye jukwaa la TPF6 kiasi kilichowafanya majaji wamuone Tanah wa kawaida, lakini siungi mkono yeye kuondolewa mapema hivyo.

Kwa upande wa Durbat aliyetolewa siku moja na Tanah, sina cha kumtetea hasa kwakuwa alionesha uanagenzi wa hali ya juu kwenye tumbuizo lake. Lawama ni kwa jopo la majaji lililompitisha kwenye usaili wa Dar. Ni kweli huo ndio mwisho wa vipaji vya Tanzania hadi yeye kuchukuliwa na kwenda kuboronga? Si kweli.

Nashindwa kueleza ni kwa kiasi gani niliumia Jumamosi baada ya Angel kutolewa. Niliumia kiasi cha usingizi wangu wa siku hiyo kuharibika. Kama shabiki wa mpira anavyoweza kuumia hadi kukataa kula chakula kwakuwa timu yake imefungwa, basi nami pia ndivyo nilivyoumia siku hiyo. Kama nilivyosema awali, matarajio makubwa siku zote hulipwa na fedheha, maumivu na uchungu.

Nakubaliana na Hermy B kuwa, kilichomponza Angel Jumamosi ni kutojiamini. Bahati mbaya ni kuwa, wasiwasi na uimbaji ni kama kuchanganya Big G na karanga, kamwe haviendani. Wasiwasi ulimfanya Angel aimbe kama mwanafunzi aliyeshika kipaza kwa mara ya kwanza. Woga ulikikandamiza kipaji cha Angel aliyekuwa tegemeo la Watanzania na akaonekana si kitu.

Kama wasemavyo waswahili kuwa ‘Siku ya kufa nyani miti yote huteleza’ ndivyo ilivyotokea Jumamosi kwakuwa washiriki hawakuruhusiwa tena kumwokoa mshiriki kama mwanzo. Huenda Angel angeliokolewa na angeendelea kushiriki.

Kingine ambacho TPF inapaswa kukibadilisha ni kuondoa utaratibu wa wasanii walioingia kwenye probation kuimba nyimbo zilezile zilizowapeleka probation. Sitaki kuamini kama msanii aliyeimba vibaya wimbo fulani atakuja auimbe vizuri ama tofauti baada ya mazoezi ya wiki moja. Chaguo baya ni baya tu. Ni sawa na kujipaka mafuta bila kuoga. Ni bora wangepewa fursa ya kuchagua nyimbo zingine na kutozirudia zile zilizowapeleka kwenye probation.

Na sasa Tanzania, imebakiza mshiriki mmoja tu. Tunamtegemea kuwa atatuokoa na aibu ya kuchekwa na wenzetu hasa katika kipindi hiki ambacho Jumuiya ya Afrika Mashariki inaendelea kuyumba. Kinachotia wasiwasi ni jinsi wenzetu wanavyotuchukulia poa kwenye shindano hilo.

Nilifurahi kuwa Jumapili hii Hisia aliimba vizuri kiasi cha kuwafurahisha majaji wote, akiwemo jaji mgumu, Ian Mbugua. Hakika aliutendea haki wimbo wa Adam Levine ft Wiz Khalifa, Payphone. Kitu kingine ni kuwa Hisia ni kipenzi cha mabinti, huenda wakamuokoa kila atakapoingia kwenye probation.

SAJENTI, MAIMARTHA WASHINDANISHA WOWOWO!


Na Richard Bukos
MWIGIZAJI Husna Idd ‘Sajent’ na mtangazaji maarufu Bongo, Maimartha Jesse wamenaswa wakishindana ukubwa wa makalio yao wakiwa wamelala kitandani.

Tukio hilo lililowashangaza wadau, lilitokea hivi karibuni wakati mastaa hao walipokuwa wanarekodi moja ya vipindi vya washiriki wa Shindano la Vigori katika Hoteli ya Kebbys Mwenge jijini Dar.

“Jamani mimi ninalo (wowowo) kuliko wewe, ukubwa dawa mimi na wewe wapi kwa wapi Sajent?” alisikika Maimartha.