Friday, February 28, 2014

MAISHA NI BUNGE, MNAJUA KUNA NINI DOM?

Nianze kwa kuwapa ‘hi’ madenti wote Tanzania nzima, anko wenu nipo katika Viwanja vya Bunge mjini Dodoma kama mmoja wa mashahidi wa nini wale wawakilishi wa makundi mbalimbali ambayo Rais Jakaya Kikwete aliwateua kujumuika pamoja kupitia rasimu ya katiba ili waweze kutengeneza katiba mpya ambayo huenda ni watoto wenu nyinyi au wajukuu zangu mimi, watakaa tena miaka 50 ijayo kuirekebisha kulingana na mazingira ya wakati huo.
Ni jambo zito sana, ingawa najua kabisa ni wachache sana kati yenu ambao mnafuatilia na kwa jinsi mnavyoishi, mimi hata sishangai. Ni rahisi nyinyi kujua kibao gani kipya Rihanna katoa, Jay Z kasema nini au Beyonce kafanya tukio gani lililovunja rekodi.
Labda niwaambie kitu kimoja. Hapa Dom, ambako ni Makao Makuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndipo niliposoma sekondari na kidogo shule ya msingi. Ninapajua kama kiganja changu. Naijua mitaa balaa, ingawa hiyo ni miaka 20 iliyopita.
Kama nilivyosema mwanzo, zaidi ya Watanzania 600 wapo hapa kujadili rasimu ya katiba iliyowasilishwa na Tume Maalum ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Sinde Warioba ambaye miaka ya nyuma, nyinyi mkiwa wadogo na baadhi yenu hamjazaliwa, alipata kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Yeye alikuwa mwenyekiti na makamu wa tume hiyo ambayo iliundwa na Rais Jakaya Kikwete.  Lakini pia ndani ya tume hiyo, walikuwepo viongozi wengi wa enzi zetu sisi, walioheshimika sana, akiwemo katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika, enzi hizo ikijulikana kama OAU, Dk. Salim Ahmed Salim.
Hawa watu walizunguka nchi nzima, kuwasikiliza wananchi wa aina na rika zote, nini wanadhani wanaona kinafaa kuwa ndani ya katiba yetu. Labda niwaulize, mnajua katiba ni nini? Najua wengi wenu hamjui, labda kama ‘Diamond Platinumz’ ataamua kuiweka katika moja ya vibao vyake, labda mtaijua.
Katiba ni sheria mama ya nchi, ndani yake haki ya kila mtu, kila kada, kila jamii imetafsiriwa. Sheria zote, zile za polisi, ardhi, misitu, mahakama na kila aina ya sheria utakayoambiwa, msingi wake mkubwa ni ndani ya katiba. Hakuna sheria wala kanuni yoyote itakayokubana wewe kama haipo ndani ya katiba hii ambayo inajadiliwa, kukubaliwa na hatimaye kutiwa saini kama sheria na wenzetu hawa wapatao 600!
Hili ni jambo kubwa sana ambalo kwa makusudi, tumekataa kulitambua uzito wake badala yake bado tunapigiana simu, kutumiana SMS, kuchati katika Facebook na Twitter kuelezana wapi leo tutakutana, wapi kuna tamasha na nani atatumbuiza!
Tukio hili ni la kihistoria, halijawahi kutokea katika nchi yetu tokea ipate uhuru mwaka 1961! Hata hao wanasiasa wakubwa mnaowasikia, hawajawahi kushuhudia utayarishwaji wa katiba mpya ya nchi yetu. Wote kwa ujumla wetu, hii ni mara ya kwanza ambayo ninaamini kabisa, kama ikienda sawa, mimi anko wenu sitashuhudia tena Watanzania wakikaa na kujadili katiba mpya!
Unajua kwa nini sitashuhudia? Hiyo labda itatokea miaka 50 ijayo. Unadhani nitakuwepo kwa maisha haya ya chipsi kuku, juisi za magumashi za Buguruni na viroba? Thubutu!
Ninachotaka kuwaambia sasa, hili jambo siyo la wale jamaa wanaosema posho ya shilingi  laki tatu kwa siku haiwatoshi, hili ni jambo lenu nyinyi maanko kwa sababu vile vibabu pale  vinawaandalia mustakabali wa maisha yenu kama taifa hapo baadaye.
Ni lazima mfuatilie kwa umakini mkubwa kinachoendelea hapa Dodoma, mjue wanawapa nini, kwa sababu baadhi yao, ambao mimi ninawapinga, eti wanataka katiba ya kulinda maisha yao ambayo imebaki miaka mitano au kumi ijayo!
Fuatilieni, hasa nyinyi ambao mpo vyuoni na hata sekondari, msikubali wawape katiba ambayo kumbe baadaye mtagundua kuwa inawalinda watoto wao, vimada wao na hata mashemeji zao. Bado hamjachelewa, mkiona wanawazingua niiteni, niambieni na mimi kwa kushirikiana na wapambanaji wenzangu, tutawapa za chembe!
Niwaage kwa kuwaambia kuwa maisha ya Dodoma wala siyo magumu kihivyo, wanatudanganya tu baadhi ya hawa wabunge. Wanasema eti shilingi laki tatu kwa siku haziwatoshi, kivipi? Nionavyo mimi hata laki moja kuimaliza kwa siku inahitaji ufujaji wa hali ya juu.
Huwa haziwatoshi labda wana myanya mingi ya matumizi, labda matanuzi yao ni ya kujionysha, isije kuwa wanawapa nyinyi madenti. Kataeni.

No comments:

Post a Comment