Saturday, June 8, 2013

Washiriki ZIFF 2013 kupigwa msasa


WAANDAAJI wa Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar (ZIFF), wameandaa warsha na kongamano kwa waandaaji na watayarishaji wa filamu 35 wanaoshiriki katika tamasha hilo linalotarajiwa kuanza Juni 29 hadi Julai 7 katika Ukumbi wa Kome Kongwe mjini Zanzibar.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam juzi, Mratibu wa tamasha hilo, Martine Mhando alisema warsha hiyo itasaidia kuongeza ujuzi katika kupiga picha, kuhariri filamu, kuigiza katika kamera, uandishi wa habari za sanaa, watoto na utengenezaji filamu.
Alisema katika tamasha hilo linalodhaminiwa na Kampuni ya Zuku, Tonya Lee Williams ambaye ni muigizaji wa kimataifa kutoka Uingereza, atakuwa mmoja wa wakufunzi na atawasaidia waigizaji na waongozaji wa filamu wa hapa nchini.
Mhando alisema tamasha hilo kwa mwaka huu litawavutia zaidi washiriki, kutokana na ZIFF kujipanga na kufanya mabadiliko makubwa mwaka hadi mwaka.
“Tunawaomba waigizaji hata ambao kazi zao hazijachaguliwa waje kushiriki warsha hii, kwani ni fursa kwao kutangaza kazi zao ambapo wanaweza kusaidiwa na Zuku katika kuzitangaza zaidi kimataifa,” alisema Mhando.
Pia alibainisha kuwa kutakuwa na jukwaa la watoto, wanawake na vijana, ambapo kutakuwa na filamu mbalimbali zitakazoonyeshwa kati ya 80 zilizochaguliwa, zikiwamo 15 za Tanzania.
Alisema mbali na warsha hizo, tamasha hilo pia linatoa nafasi kwa wasanii wa filamu kutoka nchi mbalimbali kwa kazi zao kuingia kwenye tuzo za ZIFF, ambazo zinatolewa kwa msanii aliyefanya vizuri ikiwemo tuzo ya filamu bora, msanii bora na nyingine.
“Katika tamasha mwaka huu wasanii wengi watakuwepo kutoa burudani kama Mrisho Mpoto na Mjomba Band, Skylight Band, Linah, Fid Q, Barnaba, Jhikoman, Baby J, Mkubwa na Wanawe, pamoja na wasanii wengine wengi kutoka nchi mbalimbali.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment