Monday, June 17, 2013

Askofu Kakobe: Wanaosema nimekimbia nchi wazushi

Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF) la jijini Dar es Salaam, Zachary Kakobe, amesema watu wanaomzushia amekimbia nchi na kwenda kuishi nje wana ajenda ya siri na wanastahili kukemewa ili wasijezusha jambo kubwa litakaloweza kutikisa usalama wa nchi.
Akizungumza na NIPASHE Jumapili jana jijini Dar es Salam, alisema yupo Dar es Salaam na tangu mwaka 2010 hajasafiri kwenda nje kama inavyoelezwa na baadhi ya watu kwamba amekimbia nchi.

“Uvumi huo ni wa wazushi ambao idadi yao inaelekea kuongezeka siku hizi.Wazushi hawa wamefikia hata kuwazushia watu kadhaa wakiwamo wasanii na wanasiasa kwamba wamekufa, wakati siyo kweli, sijui sababu za uzushi huu,” alisema Askofu Kakobe wakati akijibu maswali ya mwandishi kwa njia ya simu.
Alisema siku yoyote kabla ya Jumapili ya wiki hii atasafiri kwenda kufanya mkutano mkubwa wa injili jijini Toronto nchini Canada.
Kwa zaidi ya mwaka sasa kumekuwa na uvumi kwamba, Askofu Kakobe ameikimbia Tanzania na kwenda kuishi katika Jiji la Toronto, kufuatia mazingira magumu nchini katika kutangaza neno la Mungu.
Wanaozusha uvumi huo wamekuwa wakieleza sababu kadhaa zilizomfanya Askofu Kakobe kukimbia nchini kuwa ni kutokana na kukumbwa na mikasa kadhaa.
Miongoni mwa mambo yanayotajwa ni kwamba Mwaka 2007, Kakobe alikumbana na kikwazo cha kwanza baada ya serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, kufanya upanuzi wa Barabara ya Sam Nujoma kutoka Mwenge kwenda Ubungo.
Barabara hiyo ilisababisha sehemu ya maegesho ya magari nje ya kanisa lake lililopo Mwenge, jijini Dar es Salaam kumegwa. Maegesho hayo yalikuwa yakisaidia waumini wa kanisa hilo kuegesha magari yao wakati wakiwa kwenye ibada.
Mwaka 2010, kulitokea mzozo mkali kati ya Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco) ambalo lilitaka kupitisha umeme wenye msongo mkubwa wa KV 132 mbele ya kanisa la Askofu Kakobe.
Askofu Kakobe alilipinga zoezi hilo akidai licha ya madhara kwa waumini wake, umeme huo mkubwa utasumbua mitambo ya Televisheni ya Holiness aliyowaonyesha waandishi wa habari ambayo aliifunga kanisani hapo kwa ajili ya kurushia matangazo ya kiroho.  
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment